Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo ameshiriki kikao maalum cha Baraza la Madiwani kwa ajili ya kujadili hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) za mwaka 2023/2024 katika Halmashauri ya Wilaya ya Tarime na kuipongeza Halmshauri hiyo kwa makusanyo ya mapato ya ndani.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Mtambi amesema Halmashauri hiyo imekusanya jumla ya shilingi bilioni 19.1 hadi kufikia tarehe 30 Mei, 2025 kati ya lengo la kukusanya shilingi bilioni 15.3 katika bajeti ya mwaka 2024/2025.
“Bado mna mwezi mmoja mmefikisha asilimia 125 za makusanyo na bado mnaendelea kukusanya, ni imani yangu kuwa mtafanya tathmini ya mapato na kuboresha huduma kwa wananchi ili wapate maendeleo endelevu” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi ameipongeza Halmashauri hiyo kwa kupata hati safi kwa miaka mitano mfululizo na kulipongeza Baraza la Madiwani kwa kuisimamia vyema Halmashauri na kuhakikisha inapata hati safi katika kipindi chote cha uongozi wao.
Mhe. Mtambi ameliagiza Baraza la Madiwani kuisimamia Menejimenti kujibu hoja za ukaguzi na kutekeleza maagizo ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) ambayo ilitoa maagizo manne tarehe 14 agosti, 2023 ambapo Halmashauri imetekeleza agizo moja tu mpaka wakati wa kikao hicho.
Mhe. Mtambi ameiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Tarime kufuatilia na kusimamia kwa karibu matumizi za fedha zinazotekeleza miradi ya uwajibikaji kwa jamii (CSR) kutoka katika Mgodi wa Barrick North Mara ili miradi hiyo itekelezwe kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa.
Mhe. Mtambi amesema Mkoa utalifanyia kazi suala la makampuni kufanyakazi katika Mkoa wa Mara na kulipa ushuru wa huduma katika Mkoa wa Mara na sio katika maeneo mengine na kuliahidi Baraza hilo kufuatilia suala hilo kwa ukaribu.
Katika hatua nyingine, Mhe. Mtambi amekataa ombi la Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo kutaka kufanya ziara ya mafunzo kwa kutumia fedha za uwajibikaji katika jamii (CSR) zinazotolewa na mgodi wa dhahabu wa Barrick North Mara.
“Ni marufuku kutumia fedha za CSR katika ziara za mafunzo kwa Baraza la Madiwani, mkitaka mafunzo ongezeni mapato ya ndani na mtenge katika bajeti yenu ya mwaka” amesema Mhe. Mtambi na kuongeza kuwa fedha hizo zitumike kwa ajili ya miradi ya maendeleo tu.
Akitoa taarifa katika Baraza la Madiwani, Mwekahazina wa Halmashauri hiyo CPA Justin Kweka amesema katika mwaka wa ukaguzi wa 2023/2024 Halmashauri ilipata hati safi ya ukaguzi na kushukuru ushirikiano walioupata kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Wilaya ya Tarime na wadau wote katika kufanikisha Halmashauri hiyo.
CPA Kweka amesema Halmashauri ilikuwa na jumla ya hoja 64 ambapo hoja 48 ni za miaka ya nyuma kuanzia mwaka 2018/2019 wakati hoja 16 zilikuwa ni mpya hata hivyo hoja nyingi zimejibiwa na kufungwa.
Bwana Kweka amesema kwa sasa Halmashauri ina jumla ya hoja 19 na maagizo ya Kamati ya Fedha ya Serikali za Mitaa (LAAC) yalikuwa manne ambapo agizo moja limefungwa na maagizo matatu yapo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
CPA Kweka amesema Halmashauri hiyo imekuwa ikipata hati safi za ukaguzi kuanzia mwaka wa fedha 2018/2019 mfululizo hadi sasa.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime Bwana Solomon Shati amesema katika bajeti ya mwaka wa fedha 2024/2025 Halmashauri ilitenga fedha kwa ajili ya ziara ya mafunzo na tayari Baraza hilo limeshafanya ziara hiyo kwa mujibu wa bajeti.
Bwana Shati amesema Baraza la Madiwani limefanya ziara katika Halmashauri za Wilaya ya Karagwe na Muleba katika Mkoa wa Kagera na kwa sasa Halmashauri haina bajeti nyingine kwa ajili ya ziara ya madiwani.
Bwana Shati amesema katika fedha za CSR Halmashauri haikutenga fedha kwa ajili ya ziara ya Baraza la Madiwani na kufafanua kuwa sio kweli kuwa Halmashauri ilitenga fedha kwa ajili ya ziara katika bajeti ya fedha za CSR.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa