Mkuu wa Mkoa wa Mara leo tarehe 11 Juni, 2025 ameshiriki kikao maalum cha Baraza la Madiwani kwa ajili ya kujadili hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali katika Halmashauri ya Wilaya ya Rorya kwa kupata hati safi, kuongeza mapato na kupunguza hoja za ukaguzi.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Mtambi ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Rorya kwa kupata hati safi miaka minne mfululizo jambo ambalo amesema linaonyesha kuwa Halmashauri inatekeleza shughuli zake kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu.
“Ninawapongeza kwa kufanikiwa kupata hati safi za ukaguzi kwa miaka minne mfululizo na kuongeza makusanya ya mapato ya ndani na vyanzo vya mapato jambo ambalo linaonyesha mpo makini katika utendaji wenu” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi ameipongeza Halmashauri hiyo kwa kukusanya mapato ya ndani shilingi 2,215,264,387.00 hadi kufikia tarehe 30 Mei, 2025 kati ya lengo la kukusanya shilingi 2,227,047,075.00 katika lengo la mwaka wa fedha 2024/2025 ambayo ni sawa na asilimia 97 ya lengo hilo na kuitaka Halmashauri hiyo kufika asilimia 100 ifikapo tarehe 30 Juni, 2025.
Mhe. Mtambi ameipongeza Halmashauri hiyo kwa kuongeza mapato ya ndani kwa shilingi milioni 665 ikilinganishwa na makusanyo ya mwaka jana na kuongeza vyanzo vya mapato ikiwemo ujenzi wa stendi ya Mika na kuanzisha ujenzi wa soko la dagaa ili kuinua mapato ya ndani ya Halmashauri hiyo.
“Katika ukusanyaji wa mapato ninawapongeza kwa kukusanya kwa ukamilifu katika vyanzo vya awali, kuongeza vyanzo vipya vya mapato na kuendelea kutafuta vyanzo vipya vya mapato, hongereni sana” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi pia ametumia fursa hiyo kumpongeza Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rorya Mhe. Gerald Ng’onga kwa kutoa fedha shilingi milioni 19 kwa ajili ya kutengeneza magari chakavu ya Halmashauri ili Halmashauri iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
Mhe. Mtambi ameiagiza Halmashauri hiyo kulipa deni la mikopo ya madiwani katika Benki za NMB na CRDB ambao tayari Halmashauri iliwakata kutokana na posho zao lakini malipo hayo hayajawasilishwa katika Benki hizo na kuboresha usimamizi katika eneo la mununuzi ili kupunguza hoja za ukaguzi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Rorya Mhe. Dkt. Khalfan Haule amesema Wilaya inaendelea kusimamia kuhakikisha Halmashauri inapunguza hoja za ukaguzi na kuendelea kujibu hoja za zamani kwa kadiri inavyowezekana.
Mhe. Dkt. Haule amelipongeza Baraza la Madiwani kwa mafanikio makubwa ambayo Wilaya hiyo imepata na kuongeza kuwa Baraza hilo lilikuwa na madiwani 34 na kuwaombea kama ikiwapendeza wananchi wawarudishe wote kama walivyo katika uchaguzi unaofuata.
Amesema Baraza hilo limekuza makusanyo ya mapato ya ndani kutoka shilingi bilioni 1.3 hadi shilingi bilioni 2.6 mwaka huu wa fedha na shilingi bilioni tatu katika mwaka wa fedha 2025/2026 jambo ambalo amesema ni mafanikio makubwa.
Dkt. Haule ameipongeza Menejimenti kwa kuwekeza katika vyanzo vipya na endelevu vya mapato ambavyo vitaisaidia Halmashauri hiyo kupata fedha ya kujiendesha na kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi.
Mhe. Haule amesema kwa sasa Wilaya ya Rorya imeanza kuchukua hatua za kukuza kilimo na hususan mazao ya alizeti, ufuta, mbaazi, choroko na mpunga ili kuongeza kipato cha wananchi na makusanyo ya mapato ya ndani ya Halmashauri.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rorya Mhe. Gerald Samwel Ng’onga amesema katika ukaguzi wa mwaka 2023/2024 Halmashauri hiyo imepata hati safi ya ukaguzi na kuongeza kuwa tangu Baraza la Madiwani liingie madarakani Desemba, 2020 Halmashauri hiyo imekuwa ikipata hati safi.
Amesema kwa sasa Halmashauri hiyo imejikita katika kupunguza hoja za ukaguzi na katika ukaguzi huo Halmashauri ya Wilaya ya Rorya imepata hoja mpya 19 tu na kuongeza kuwa awali ilikuwa inapata hoja nyingi kila mwaka.
Mhe. Ng’onga amesema kwa sasa Halmashauri hiyo inazo hoja 88 na kati ya hizo hoja 64 ni za miaka ya nyumba, maagizo ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) matano na hoja 19 ni mpya na kuongeza kuwa hoja hizo nyingi zimejibiwa na zinaweza kufungwa baada ya wakaguzi kufanya uhakiki wa majibu hayo.
Kikao hicho kilihudhuriwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, Kamati ya Usalama ya Wilaya ya Rorya, baadhi ya watumishi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, Madiwani na Menejimenti ya Halmashauri ya Wilaya ya Rorya.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa