Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Evans Alfred Mtambi leo tarehe 13 Juni, 2025 ameshiriki kikao maalum cha Baraza la Madiwani kwa ajili ya kujadili hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika Halmashauri ya Mji wa Bunda na kuipongeza halmashauri hiyo kwa kupata hati safi ya ukaguzi.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Mtambi ameipongeza Halmashauri hiyo kwa kupata hati safi kwa miaka mitano mfululizo na namna ambavyo Halmashauri hiyo imepata hoja chache za ukaguzi.
“Sote tumeshuhudia umahiri wao uliosababisha wawe na hoja chache za ukaguzi ukilinganisha na Halmashauri nyingine za Mkoa wa Mara ambazo zinahoja nyingi” amesema Mhe. Mtambi na kuipongeza Halmashauri hiyo ina kwa kuwa na hoja 12 tu zinazoendelea.
Mhe. Mtambi amepongeza Baraza la Madiwani, Menejimenti na watumishi wote kwa ukusanyaji wa mapato ya ndani ambapo amesema hadi kufikia tarehe 30 Mei, 2025 Halmashauri hiyo imekusanya shilingi 2,536,906,322 ambayo ni sawa na asilimia 98 ya lengo la makusanyo yaliyotarajiwa katika mwaka wa fedha 2024/2025.
Mhe. Mtambi amesema kuwa anayo matumaini makubwa kuwa Halmashauri hiyoi itafika asilimia 100 au zaidi ifikapo 30 Juni, 2025 na kuongeza kuwa makusanyo hayo yataiwezesha Halmashauri kutekeleza mipango yake iliyowekwa katika bajeti hiyo kwa ufanisi.
Mhe. Mtambi amelitaka Baraza la Madiwani kuisimamia Halmashauri kuandaa mpango mkakati wa kutekeleza maagizo matatu yaliyotolewa na Kamati ya Bunge ya Fedha za Serikali za Mitaa (LAAC) na hoja zilizobakia za ukaguzi.
Kanali Mtambi ameitaka Halmashauri hiyo kuongeza ubunifu katika kuibua vyanzo vipya vya mapato ikiwa ni pamoja na kufanya upembuzi yakinifu kubaini haki na stahiki za Halmashauri katika uwekezaji unaofanyika katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti (SENAPA).
Mhe. Mtambi ameitaka Halmashauri kuhakikisha fedha zinazokusanywa zinapelekwa benki, manunuzi yanafanyika kupitia mfumo wa NEST na dawa na vifaa tiba vinanunuliwa Bohari ya Dawa (MSD) kwa kutumia utaratibu uliowekwa na Serikali.
Mhe. Mtambi ameitaka Halmashauri ya Mji wa Bunda kukaa na Halmashauri ya Wilaya ya Bunda ili kujadili mgawanyo wa mali na madeni kati ya Halmashauri hizo na kuwakumbusha kuwa agizo hilo alilitoa mwaka jana na hawakutekeleza, na ametoa siku 30 kuanzia leo na apate taarifa ya utekelezaji.
Mhe. Mtambi amemtaka Mkuu wa Wilaya ya Bunda kusimamia suala la mgawanyo wa mali na madeni ya Halmashauri hizo na kuwasilisha taarifa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara ndani ya siku 30.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Bunda Mhe. Aswege Enock Kaminyoge amesema kulikuwa na tatizo la uvamizi wa tembo katika Kata za Balili, Buzugu na Hunyari ambao walisababisha kifo cha kijana mmoja na kuharibu mali za wananchi.
Mhe. Kaminyonge amesema kufuatia tatizo hilo, Wilaya kwa kushirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA) ilichukua hatua ikiwa ni pamoja na kutoa pole katika familia ya marehemu na kuzungumza na wananchi wa maeneo yaliyoathirika.
Mhe. Kaminyoge amesema Wilaya imetoa maagizo kwa TAWA, Shirila la Hifadhi za Taifa (TANAPA) na Grumeti kufanya operesheni maalum kuhakikisha tembo hawasogei katika maeneo ya wananchi na hususan Katika kipindi hiki ambapo tembo wanafuata mazao kama vile mpunga na mihogo.
Mhe. Keminyonge amesema Wilaya ya Bunda inaendelea kusimamia utoaji wa chakula shuleni, kuhakikisha kuna madawati na ukarabati wa shule kongwe ili kuimarisha mazingira ya utoaji wa elimu katika Wilaya hiyo ili kuinua ufaulu wa wanafunzi.
Akiwasilisha taarifa yake, Mwekahazina wa Halmashauri ya Mji wa Bunda CPA Antonia Ndawi amesema Halmashauri ya Mji wa Bunda katika ukaguzi wa mwaka wa fedha 2023/2024 imepata hati safi kwa taarifa zote tatu yaani taarifa ya ujumla, mfuko wa pamoja wa afya, na mfuko wa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
CPA Ndawi amesema kwa mwaka wa fedha 2023/2024 Halmashauri ilikuwa na hoja 21 na kati ya hoja hizo hoja 16 zimetokana na taarifa ya jumla, hoja nne zimetokana na mfuko wa pamoja wa afya na hoja moja ya mfuko wa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu na kati ya hoja hizo tano zimejibiwa na kushafungwa.
Aidha, CPA Ndawi amesema Halmashauri pia ilikuwa na hoja za nyuma 16 kati ya hizo hoja tatu zimefungwa, hoja mbili zimepitwa na wakati na hoja 11 ambazo utekelezaji wake unahitaji uwepo wa fedha.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Bunda Mhe. Michael Kweka amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Marakwa ushirikiano wake alioutoa katika Baraza hilo na kushukuru ushirikiano kati ya madiwani, menejimenti na watumishi wa Halmashauri hiyo.
Mhe. Kweka amesema Halmashauri ya Mji wa Bunda imefanyakazi kubwa kuhakikisha inakusanya mapato kwa asilimia kubwa na kwa sasa wanatarajia kufikisha asilimia 110 hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2025 ili kuwatumikia wananchi wa Mji wa Bunda.
Mhe. Kweka amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuleta fedha za kutekeleza miradi mingi katika Halmashauri hiyo na kukihakikishia kikao kuwa utekelezaji wa ilani umefanyika vizuri na anauhakika kutokana na kazi iliyofanyika madiwani wa Halmashauri hiyo watachaguliwa na wananchi kurejea kuwatumikia katika uchaguzi ujao.
Kikao hicho kilihudhuriwa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, Kamati ya Usalama ya Wilaya ya Bunda, baadhi ya watumishi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, Madiwani na Menejimenti ya Halmashauri ya Mji wa Bunda.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa