Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Ndugu Gerald Musabila Kusaya leo ameshiriki maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani katika Halmashauri ya Wilaya ya Musoma na kuwataka wauguzi kuishi viapo vyao wanapotoa huduma kwa wananchi.
Ndugu Kusaya amesema wauguzi wameapa mbele ya umma kutoa huduma bora na kuongeza kuwa kauli mbiu ya siku ya waguuzi mwaka huu ni “Uuguzi ni nguvu ya kuleta Mabadiliko Duniani” na kuwataaka kuiishi kauli hiyo kwa vitendo ili kuokoa maisha ya wananchi.
“Viapo vyenu ambavyo mnakuwa mnavirudia mara kwa mara ni vizuri sana na kama mkiviishi kwa vitendo vitaokoa maisha ya wananchi wengi katika maeneo yenu” amesema Bwana Kusaya.
Ndugu Kusaya amewataka wananchi kutoa ushirikiano kwa wataalamu wa afya wakiwemo wauguzi ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kuyafanyia kazi mambo mbalimbali wanayoelekeza katika jamii ikiwemo kuzingatia lishe, usafi wa mazingira na kufanya mazoezi.
Akizungumzia kuhusu upungufu wa watumishi Ndugu Kusaya amesema upungufu wa watumishi upo katika sekta mbalimbali sio sekta ya afya pekee na kuongeza kuwa kwa sasa Mkoa wa Mara unahitaji watumishi 15,441 wa kada mbalimbali.
“Serikali imekuwa ikiajiri watumishi mara kwa mara na kwa mwaka huu pekee Halmashauri ya Wilaya ya Musoma imepokea watumishi 170 na kati yao watumishi 48 wakiwa wa sekta ya afya” amesema Bwana Kusaya.
Aidha, Bwana Kusaya amesema Halmashauri imepokea kibali cha ajira kwa watumishi 40 na baadhi yao watakuwa ni wa sekta ya afya wakiwemo wauguzi.
Bwana Kusaya ametumia fursa hiyo kuipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Musoma kwa kutenga shilingi milioni 50 kwa mwaka kwa ajili ya kununua vifaa tiba kwa ajili ya vituo vya kutolea huduma za afya.
Bwana Kusaya ametumia fursa hiyo pia kuwahamasisha wananchi na watumishi kushiriki uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 na kuwataka watumishi wanaotaka kugombea katika uchaguzi huo kufuata taratibu za kiutumishi kuaga ili waweze kuruhusiwa kuondoka.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma Bwana Msongera Palera amesema Halmashauri inaupungufu wa watumishi lakini Serikali imekuwa ikileta watumishi kila mwaka kutatua changamoto hiyo.
Bwana Palera amelishukuru Baraza la Madiwani kwa ushirikiano na maamuzi mazuri wanayotoa na kuwapongeza wauguzi kwa kazi nzuri wanayoifanya na kuwahakikishia watumishi wenye madai ya malimbikizo ya mshahara madai yao yapo katika hatua nzuri muda wowote wanaweza kulipwa.
Bwana Palera amesema kuhusu malipo ya posho, unifomu na stahiki nyingine ameviachia vituo ili vilipe kulingana na makusanyo katika vituo na kuwataka watumishi kuboresha huduma zao ili kuongeza makusanyo.
Kwa upande wake, Kaimu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma Mhe. Mussa Munubi amemuomba Katibu Tawala wa Mkoa kuisaidia Halmashauri katika kutatua tatizo la watumishi wa sekta ya afya katika Halmashauri hiyo.
“Mahitaji ni watumishi 223 na kwa sasa waliopo ni watumishi 104 tu na hivyo kuna upungufu wa watumishi 119 na upungufu mkubwa ukiwepo hapa katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Musoma” amesema Mhe. Munubi.
Mhe. Munubi amewapongeza watumishi kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na uchache wao na kuwataka kuendelea kufanya kazi kwa bidi ili kuokoa maisha ya wananchi wa Musoma wanaotegemea huduma za afya kutoka kwa wataalamu hao.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wauguzi Tanzania (TANA) Halmashauri ya Wilaya ya Musoma Bibi Nice Mremi amesema wauguzi ndio wataalamu wanaompokea mgonjwa na wataalamu wa mwisho kuagana na mgonjwa na kuiomba Serikali kuwaboreshea mazingira yao ya kufanyia kazi.
Bibi Mremi ameomba Serikali kuongeza idadi ya watumishi na hususan Hospitali ya Halmashauri, vitendea kazi, fedha za sare, likizo na posho zitolewe kwa wakati, kuboresha baadhi ya vituo vya kutolea huduma.
Kwa upande wake, Bwana Ndulu Mahera, Mratibu wa Maabara Halmashauri ya Wilaya ya Musoma amesema katika kuadhimisha wiki ya wauguzi, Halmashauri iliweka mahema na kufanya upimaji wa baadhi ya magonjwa na kutoa chanjo na ushauri nasaha kwa wananchi katika viwanja hivyo.
Bwana Mahera amesema wamefanikiwa kuhamasisha wananchi 46 kuchangia damu, wamepima UKIMWI watu 45, wametoa chanjo mbalimbali kwa watoto na kutoa ushauri kuhusiana na uzazi wa mpango kwa wananchi.
Katika maadhimisho hayo, Katibu Tawala amezindua kampeni ya lishe katika Halmashauri hiyo, amegawa zawadi kwa wagonjwa zilizotolewa na waauguzi na ameendesha harambee fupi ya kutunisha mfuko wa Chama cha Wauguzi.
Maadhimisho hayo yamehudhuriwa na baadhi ya Watumishi kutoka Sekretarieti ya Mkoa wa Mara, Kaimu Mwenyekiti wa Halmashauri, Mkurugenzi wa Halmashauri, watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma na wananchi wa maeneo hayo.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa