Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Bwana Gerald Musabila Kusaya amewataka wananchi waliopata madhara yaliyosababishwa na mvua iliyoambatana na upepo katika Manispaa ya Musoma tarehe 23 Machi, 2025 kutumia misaada wanayopewa kuboresha maisha yao.
Akizungumza katika hafla ya kukabidhi misaada kwa wahanga amewataka kutumia misaada hiyo kwa malengo yaliyokusudiwa ili kuboresha maisha yao baada ya tatizo hilo lililowapata.
“Msaada mtakaopokea leo msiende kutumia ovyo, mtumie kulingana na malengo ya misaada hiyo katika kuboresha maisha yenu baada ya masaibu yaliyowakuta” amesema Bwana Kusaya.
Bwana Kusaya amemshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kutoa fedha na vifaa kama vile mabati, magodogo, mablanketi, ndoo kwa ajili ya waathirika hao.
Aidha, amewashukuru Mbunge wa Viti Maalum Ghati Chomete, Mbunge wa Jimbo la Musoma Mjini Mhe. Vedastus Mathayo, Nyansaho Foundation, mgodi wa Barrick North Mara na wadau wengine waliotoa msaada kwa waathirika hao kwa nyakati tofauti.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Mara Mhe. Juma Chikoka amesema anaishukuru Serikali na wadau wote waliochangia katika maafa hayo na kuwashukuru wananchi kwa ustahimilivu wao wakati Serikali ilipokuwa inatoa msaada kwa makundi mbalimbali kulingana na uathirika wao.
Mhe. Chikoka amewahakikishia wananchi hao kila mmoja aliyeathirika atafikiwa na Serikali na kupewa msaada kulingana na kiasi cha fedha na mali zilizopo.
Mhe. Chikoka amewataka wananchi kuendelea na shughuli zao za maendeleo kwa amani na utulivu wakati huu nchi inapoelekea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 na kuwahakikishia kuwa usalama wakati wote wa uchaguzi.
Kwa upande wake, Mratibu wa Maafa Manispaa ya Musoma Bibi Aines Anderson amesema katika maafa hayo nyumba 196 ziliathirika na kusababisha kaya 139 kukosa makazi na kaya 16 zenye watu 40 zilihifadhiwa katika majengo ya NFRA na kuhudumiwa kwa chakula na malazi kwa siku tatu kabla ya kupewa pesa za pango la miezi sita kwa kila kaya.
Bibi Aines Anderson amesema tangu kutokea kwa maafa hayo, jumla ya nyumba sita za wazee na watu wasiojiweza zimejengwa katika kata za Nyakato, Kitaji, Kwangwa na Rwamlimi na kukarabati nyumba 33 katika kata za Kitaji na Nyakato.
Amesema msaada unaogawiwa leo ni mabati 568 kwa ajili ya kaya 29, magodoro 91 na mablanketi 100 yaliyotolewa kwa ajili ya kaya 91 na saruji mifuko 70 iliyotolewa kwa ajili ya jengo la kilimo na Shule ya Msingi Mwembeni B zilizoathirika katika tukio hilo.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa