Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo amezitaka Halmashauri kuongeza ubunifu katika kupanua vyanzo vya mapato ya ndani ya Halmashauri ili kuziwezesha Halmashauri kujiendesha na kutekeleza miradi ya maendeleo kwa wananchi.
Mhe. Mtambi ametoa kauli hiyo wakati akizungumza katika Baraza la Madiwani kuhusu hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali katika Halmashauri ya Wilaya ya Musoma na kukumbushia agizo lake kwa Halmashauri hiyo kuanzisha mnada na gulio katika maeneo ya wachimbaji wadogo katika Halmashauri hiyo.
“Mimi niliagiza kuanzisha gulio au mnada katika maeneo ya wachimbaji wadogo ambayo yana watu wengi ili kutumia fursa hiyo kutoa huduma kwa wananchi na kuwa chanzo cha mapato kwa Halmashauri, tekelezeni agizo hilo” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi amezitaka Halmashauri kuweka nguvu katika miradi ya maendeleo itakayowasaidia wananchi kupata huduma na kuibua fursa za biashara hata kama wakati mwingine Halmashauri zinaona hamna faida kwa Halmashauri kwa wakati ule ili kuwasaidia wananchi.
Ameitaka Halmashauri hiyo kuona uwezekano wa kuanzisha Samaki Festival na kuitangaza vizuri ili kuwa sehemu ya wananchi kupumzika na kufanya biashara mbalimbali ikiwemo biashara ya samaki.
Mkuu wa Mkoa ameitaka Halmashauri hiyo kuhakikisha fedha zote zinazokusanywa kupelekwa benki kwa wakati na kuwachukulia hatua watu wote wanaochelewesha kupeleka benki makusanyo kwa mujibu wa taratibu za fedha na kuhakikisha manunuzi yote yanafanyika kupitia mfumo wa NEST.
Kanali Mtambi ameitaka Halmashauri ya Wilaya ya Musoma kuendelea kutoa elimu na hamasa kwa vijana ili waweze kuchangamkia fursa za mikopo inayotolewa na Halmashauri ili kujikwamua kiuchumi na kukuza ajira katika maeneo yao.
Wakati huo huo, Mhe. Mtambi pia ameipongeza Halmashauri hiyo kwa mwenendo wake wa makusanyo ya ndani ambapo hadi kufikia tarehe 30 Mei, 2025 ilikuwa imekusanya shilingi bilioni 2.2 ambayo ni zaidi ya asilimia 93 ya lengo lake la kukusanya shilingi bilioni 2.3 katika mwaka wa fedha 2024/2025.
“Hii inaonyesha kuwa mnaweza kuvuka lengo kama mkijipanga vizuri katika makusanyo. Ninatamani itakapofika tarehe 30 Juni, 2025 Halmashauri iwe imekusanya kwa zaidi ya asilimia 100” amesema Mhe. Mtambi.
Aidha, ameipongeza Halmashauri hiyo kwa kuvuka lengo la makusanyo katika mwaka wa fedha 2024/2025 ambapo Halmashauri ilifanikiwa kukusanya asilimia 105 ya lengo lake la makusanyo na kuwahamasisha kuvuka lengo kwa mwaka huu pia.
Mhe. Mtambi amesema Halmashauri hiyo ikiongeza juhudi katika ukusanyaji wa mapato ya ndani itaweza kutekeleza miradi mingi ya maendeleo kwa wananchi na kuinua huduma muhimu kwa wananchi wa Halamshaur hiyo.
Awali akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Mhe. Charles Manumbu amesema Halmashauri hiyo imekuwa ikiboresha makusanyo yake mara kwa mara na wakati yeye anaingia mwaka 2015 ilikuwa inakusanya shilingi milioni 600 tu lakini kwa sasa tumefika zaidi ya bilioni mbili.
Mhe. Manumbu amesema kwa mwaka wa fedha 2025/2026 Halmashauri hiyo inapanga kukusanya shilingi bilioni 2.6 kama mapato ya vyanzo vya ndani baada ya kufanikiwa kukusanya bilioni vizuri kwa mwaka uliopita na mwaka huu wa 2024/2025.
Mhe. Manumbu amesema Baraza la Madiwani limeshaazimia kukusanya mapato zaidi ili Halmashauri hiyo iweze kurudishwa kwenye Halmashauri zinazopeleka asilimia 40 ya fedha zake katika miradi ya maendeleo ili kuwaboresha huduma kwa wananchi.
Mhe. Manumbu amepongeza ushirikiano mkubwa walioupata katika Halmashauri hiyo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Watumishi na Baraza la Madiwani katika kutekeleza mipango na miradi mbalimbali iliyotekelezwa katika Halmashauri hiyo.
Baraza Maalum la Madiwani limehudhuriwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, wajumbe wa Kamati ya Usalama wa Wilaya ya Musoma, baadhi ya watumishi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, maafisa kutoka ofisi ya CAG, Menejimenti ya Halmashauri ya Wilaya ya Musoma.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa