Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 11 Aprili, 2025 ametembelea mradi wa ukarabati na upanuzi wa Uwanja wa Ndege Musoma uliopo katika Kata ya Mkendo, Manispaa ya Musoma na kuzitaka taasisi zote zinazohusika na mradi huo kuhakikisha unakamilika kabla ya Septemba, 2025.
Akizungumza baada ya kupokea taarifa za maendeleo ya upanuzi na ukarabati huo, Mhe. Mtambi amesema tayari Serikali imetoa fedha za ukamilishaji wa uwanja huo na kwa kasi aliyoiona katika uwanja huo haoni sababu ya uwanja huo kutokukamilika mapema.
“Taarifa yenu na hali halisi ya utekelezaji wa mradi huu inaonyesha kuwa unaweza kukamilika kabla ya septemba, angalieni mtakachoweza kufanya ili mradi huu ukamilike mapema kutokana na umuhimu wake kwa Mkoa wa Mara” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi amesema uwanja huo utakapokamilika utasaidia sana katika kuwasafirisha wananchi, watalii, madini, samaki na mizigo mingine kutoka Mkoa wa Mara kwa urahisi na haraka na utasaidia katika kukuza uchumi wa Mkoa wa Mara.
Mhe. Mtambi ameipongeza TANROADS Mkoa wa Mara kwa usimamizi mzuri wa mradi huo na kuitaka ihakikishe inakamilisha mradi huo kwa wakati na kumtaka Mkandarasi wa mradi huo kukamilisha shughuli zilizobakia ili uwanja uweze kutumika.
Mhe. Mtambi amemtaka Meneja wa Uwanja wa Ndege Musoma kufuatilia mchakato wa ujenzi wa majengo mapya ya abiria kwa ukaribu huku akiendelea kufanya maandalizi ya kuanza kupokea ndege za abiria katika majengo ya zamani ya abiria yaliyopo katika uwanja huo.
Kanali Mtambi amemtaka Mkuu wa Wilaya ya Musoma Mhe. Juma Chikoka kufuatilia utekelezaji wa mradi huo kwa karibu na kuongeza kuwa mradi huo ukikamilika utaichangamsha sana Manispaa ya Musoma na Mkoa wa Mara kwa ujumla kibiashara na utalii.
Kwa upande wake, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Mara Mhandisi Vedastus Maribe amesema awali mradi huo ulisimama kutokana na Mkandarasi kudai malipo yake baada ya kukamilisha sehemu ya kazi, lakini kwa sasa Mkandarasi ameshalipwa asilimia 80 ya fedha zote na anaendelea na ukamilishaji wa mradi.
“Utekelezaji wa mradi unaendelea vizuri na sasa umefikia asilimia 58 ya utekelezaji wa jumla wa mradi huu na tunatarajia kuukamilisha mwezi Septemba, mwaka huu” amesema Mhandisi Maribe.
Mhandisi Maribe amesema wananchi wote waliotakiwa kulipwa fidia ili kupisha mradi wameshalipwa na wanaendelea na maandalizi ya kuhama katika eneo hilo ili upanuzi wa uwanja huo uweze kuendelea.
Kwa upande wake, Meneja wa Uwanja wa Ndege Musoma kutoka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Frank Msofe amesema taratibu za kukarabati na kuweka sawa majengo yaliyopo kwa ajili ya kutumika kupokea abiria zinaendelea wakati wakisubiria ujenzi wa majengo ya kisasa ya abiria katika uwanja huo.
Bwana Msofe amesema tayari Serikali imeanza mchakato wa kuwalipa wananchi 58 fidia ya zaidi ya shilingi bilioni tano kwa ajili ya kupisha ujenzi wa majengo ya kisasa ya kupokelea abiria katika uwanja huo.
Bwana Msofe amesema baada ya wananchi kulipwa fidia hizo, TAA itajenga majengo ya kisasa ya abiria katika uwanja huo ili abiria watakaotumia uwanja huo waweze kuhudumiwa vizuri zaidi.
Katika ziara hiyo, Mhe. Mtambi ameambatana na Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Maafisa kutoka Sekretarieti ya Mkoa wa Mara, TANROADS, TAA, na Wakandarasi na wazabuni wanaotekeleza miradi huo.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Postal Address: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Telephone: +255282622305
Mobile:
Email: ras.mara@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Mara Region . All rights reserved.