Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Evans Alfred Mtambi leo tarehe 05 Juni, 2025 akiwa ameambatana na Kamati ya Usalama ya Mkoa amezungumza na viongozi wa dini na Kamati ya Amani na Maridhiano ya Mkoa wa Mara na kuwataka kuendelea kuomba na kuhubiri amani hususan Taifa linapoelekea katika uchaguzi Mkuu.
Mhe. Mtambi amewataka viongozi wa dini kuwahamasisha waumini waweze kuchangamkia fursa zilizopo katika Mkoa wa Mara ili waweze kutafuta fedha za kufanya maendeleo yao ili kuimarisha uchumi wao na jamii kwa ujumla.
“Jamii ikiwa na nguvu ya kiuchumi inakuwa rahisi zaidi kuihubiria suala la amani na usalama kwa kuwa hamna anayeweza kushawishika kirahisi kujiunga katika makundi yasiyofaa” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi amewataka viongozi wa Dini kuuombea Mkoa wa Mara na nchi yetu Tanzania ili uchaguzi ufanyike kwa amani na utulivu na maisha ya wananchi yaendelee vizuri baada ya uchaguzi.
Mhe. Mtambi amewataka viongozi wa Dini kukemea uvunjifu wa maadili katika jamii na kukemea mauaji ya kirejareja ya wananchi yanayotokana sababu mbalimbali ikiwemo wivu wa mapenzi na migogoro mingine katika jamii ambayo ingeweza kusuluhishwa bila kuwepo kwa mauaji hayo.
Mhe. Mtambi amewashukuru viongozi wa dini kwa kuendelea kukemea vitendo vya uvunjifu wa amani katika jamii na kwa sasa Mkoa wa Mara unafanya vizuri kulingana na takwimu zinazotolewa na Wizara ya Mambo ya Ndani inaonyesha kuwa Mkoa wa Mara haupo katika mikoa 10 inayoongoza kwa uhalifu hapa nchini.
“Mchango wenu katika kuleta haya mabadiliko ya kijamii na kuacha vitendo vya uhalifu na unyanyasaji ni mkubwa sana na kama Mkoa tunauthamini sana” amesema Mhe. Mtambi na kuongeza kuwa Dini ni chombo pekee kinachoweza kumpunguzia mtu msongo wa mawazo.
Aidha, amewataka kukemea matendo maovu kama vile mapenzi ya jinsia moja, ukeketaji na migogoro katika jamii na kuwahamasisha waumini kuishi maisha ya kindugu na mshikamano wa kijamii katika maeneo yao.
Kikao hicho kimehudhuriwa na viongozi wa Dini, Kamati ya Usalama ya Mkoa wa Mara na baadhi ya watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa