Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi ameshiriki Baraza Maalum la Madiwani linalojadili hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali katika Manispaa ya Musoma na kuipongeza Manispaa hiyo kwa kupata hati safi kwa miaka mitano mfululizo.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Mtambi amelipongeza Baraza la Madiwani, Menejimenti, watumishi wa Manispaa hiyo na wadau wote waliohusika katika kuiwezesha Manispaa kupata hati safi ya ukaguzi.
“Hii inaonyesha Manispaa ina uimara wa mifumo ya usimamizi wa mapato na matumizi ya Manispaa na juhudi za kila mmoja katika utekelezaji wa majukumu” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi amelitaka Baraza la Madiwani kusimamia kasoro za usimamizi wa mikataba na manunuzi ili thamani ya fedha katika miradi iweze kuonekana na kuhakikisha manunuzi yote yanafanyika kupitia mfumo wa ununuzi na kupunguza hoja za ukaguzi katika Manispaa hiyo.
Kanali Mtambi ameiagiza Halmashauri ya Manispaa ya Musoma kuandaa mkakati wa kumaliza hoja za ukaguzi na maagizo ya LAAC na kuuwasilisha ofisini kwake tarehe 30 Juni, 2025 na kuhakikisha maafisa wanaosababisha hoja wanachukuliwa hatua za kiutumishi.
Mhe. Mtambi ametoa wiki mbili kwa Katibu Tawala Mkoa wa Mara kumrejesha Bashiri Gasori aliyekuwa Afisa Uvuvi wa Manispaa hiyo na baadaye kuhamia Manispaa ya Ilemela baada ya kubainika kuwa uhamisho wake haukuwa halali.
Mhe. Mtambi amesema hali ya ukusanyaji wa mapato katika Manispaa ya Musoma hairidhishi na kuitaka kuweka mikakati ya kuongeza vyanzo vya mapato na kukusanya mapato kwa ufanisi ili kupata fedha za kuiendesha Halmashauri na kutekeleza miradi ya maendeleo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Musoma Mhe. Juma Chikoka amesema hoja nyingi za Halmashauri hiyo zilipaswa kuwa zimefungwa kwa sababu majibu ya hoja nyingi kati ya hizo yapo wazi na ndani ya uwezo wa Manispaa kujibu.
Mhe. Chikoka amesema Manispaa hiyo itaandaa utaratibu wa kuwatambua ni maafisa gani wanaowasababishia hoja za ukaguzi watawachukulia hatua na kuwataka watumishi kila mtu atimize wajibu wake.
Mhe. Chikoka amesema Wilaya ya Musoma itasimamia uandaaji wa mkakati wa kukamilisha hoja za ukaguzi na itahakikisha Manispaa inawasilisha mkakati huo kabla ya tarehe 30 Juni, 2025 na inafunga hoja nyingi ambazo majibu yake yamo ndani ya uwezo wa Manispaa.
Kwa upande wake, Mwekahazina wa Manispaa ya Musoma ACPA Emmanuel Abraham amesema katika mwaka wa fedha 2023/2024 Halmashauri ilikuwa na hoja 72 na baada ya uhakiki hoja 37 zimefungwa huku hoja nyingine 48 zikiendelea kufayiwa kazi.
Aidha, Bwana Abraham amesema Manispaa ilikuwa na maagizo saba ya Kamati ya Bunge ya Fedha za Serikali za Mitaa (LAAC) ambapo maagizo mawili yamefungwa na maagizo matano yanaendelea kufanyiwa kazi.
Bwana Abraham amesema pamoja na HAlmashauri hiyo kupata changamoto ya kufunga hesabu katika mfumo wa uhasibu serikalini (MUSE) lakini baada ya hesabu hizo kufungwa imepata hati safi ya ukaguzi.
Kikao hicho kilihudhuriwa na Katibu Tawala Mkoa wa Mara, Kamati ya Usalama ya Wilaya ya Musoma, Maafisa kutoka ofisi za ukaguzi na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, madiwani na menejimenti ya Manispaa ya Musoma.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa