Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Evans Alfred Mtambi leo tarehe 23 Juni, 2025 amewapokea na kufungua rasmi kambi ya madaktari bingwa na bobezi 64 watakaotoa huduma katika Hospitali za Halmashauri za Mkoa wa Mara kwa siku tano kuanzia leo tarehe 23 Juni, 2025 hadi tarehe 27 Juni, 2025 na kuwataka wananchi kuchangamkia fursa hiyo.
Akizungumza katika mapokezi hayo, Mhe. Mtambi amesema kazi kubwa ya madaktari hayo watakayoifanya ni kuokoa maisha ya wananchi ambao wanahitaji matibabu ya kibingwa na hawana uwezo wa kwenda hospitali za rufaa zilizopo.
“Ninawaomba wananchi kujitokeza kwa wingi kuwapeleka wagonjwa kupata huduma za kibingwa na bobezi katika hospitali za Halmashauri na kutumia fursa hii vizuri” amesema Mhe. Mtambi.
Kanali Mtambi amesema Serikali ya awamu ya sita iwemekeza sana katika sekta ya afya na kwa sasa Hospitali za Halmashauri zinamazingira mazuri na vifaa tiba vya kuwawezesha Madaktari bingwa na bobezi kutoa huduma za kibingwa katika hospitali hizo.
Mhe. Mtambi ametumia fursa hiyo kuwakaribisha Madaktari Bingwa na Bobezi katika Mkoa wa Mara na kuwataka kutembelea Makumbusho na nyumbani kwa Baba wa Taifa, Butiama, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na kula nyama choma na kichuri.
Kwa upande wake, Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii Dkt. Zabron Masatu amesema Mkoa umepokea madaktari bingwa na bobezi 64 ambapo kila Halmashauri itapata madaktari bingwa na bobezi saba na Manispaa ya Musoma itapata Madaktari Bingwa na Bobezi nane.
Dkt. Masatu amesema katika mwezi wa Novemba, 2024 Mkoa ulipokea timu ya madaktari Bingwa na Bobezi ambao walifanikiwa kutibu wagonjwa 4,287 na kati yao 476 walilazwa ili kutibiwa zaidi, 259 walifanyiwa upasuaji na 203 walipewa rufaa za matibabu katika Hospitali za Rufaa za Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere na Hospitali ya Rufaa ya Bugando.
Dkt. Masatu amesema kutokana na matangazo yanayoendelea katika Halmashauri zote za Mkoa wa Mara wanategemea watu wengi wamepata taarifa na watachangamkia fursa hiyo kupata matibabu.
Kwa upande wake, Mratibu wa Huduma Mkoba kutoka Wizara ya Afya Dkt. John Mwombeki amesema madaktari bingwa na bobezi wakiwa katika Mkoa wa Mara watafanyakazi katika Hospitali za Halmashauri ili kutoa matibabu ya kibingwa kwa wagonjwa.
Dkt. Mwombeki amesema wakiwa huko, wataalamu hao watawajengea uwezo wataalamu wa afya watakaowakuta katika maeneo hayo kuhusiana na tiba watakazozitoa kwa wagonjwa na kuwafundisha kuhusu matumizi ya vifaa tiba vilivyopo katika hospitali hizo.
Dkt. Mwombeki amesema sambamba na uwepo wa madaktari bingwa na bobezi hao, wataalamu kutoka Taasisi ya Utafiti wa Huduma za Afya (NIMRI) ambao wakuwa wanafanya utafiti kuhusiana na huduma za matibabu katika Halmashauri za Mkoa wa Mara.
Hospitali zitakazohusika na kambi hii ni Hospitali ya Manispaa ya Musoma, Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Butiama, Hospitali ya Manyamanyama (Bunda), Hospitali ya Wilaya ya Serengeti, Hospitali ya Wilaya ya Tarime (Nyamwaga), Hospitali ya Mji wa Tarime (Bomani), Hospitali ya Wilaya ya Bunda (Bukama) na Hospitali ya Wilaya ya Rorya.
Madaktari hao ni bingwa katika magonjwa ya ndani, mikojo na upasuaji, magonjwa ya akina mama, watoto, macho, kinywa na meno, pua, koo na masikio na magonjwa ya mifupa pamoja na wataalamu wa dawa za usingizi na wauguzi wabobezi.
Hafla ya mapokezi ya madaktari hao imehudhuriwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Ndugu Gerald Musabila Kusaya, Menejimenti ya Sekretarieti ya Mkoa wa Mara, Maafisa kutoka Wizara ya Afya, Wajumbe wa Kamati ya Usimamizi wa Afya Mkoa wa Mara (RHMT), Wakuu wa Divisheni za Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii wa Halmashauri na Madaktari Bingwa.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa