Mkuu wa Wilaya ya Rorya Mhe. Dkt. Khalfan Haule amewataka wadau wa zao la tumbaku kuzingatia miongozo na kanuni za kilimo cha zao la tumbaku ili kuongeza uzalishaji na kuboresha hali ya wakulima wa zao hilo.
Mhe. Haule ametoa kauli hiyo wakati wa mkutano wa kwanza wa wadau wa zao la tumbaku uliowaleta pamoja wakulima, wanunuzi, wawakilishi wa Serikali na taasisi za kifedha katika Mkoa wa Mara uliofanyika tarehe 17 Juni, 2025 katika Hoteli ya Kisare iliyopo katika Mji wa Mugumu, Wilaya ya Serengeti.
“Mafanikio katika kilimo cha tumbaku yanategemea sana kufuatwa kwa taratibu za ulimaji na uvunaji wa zao hilo ili kuleta manufaa makubwa kwa mkulima kama inavyokusudiwa, bila hivyo wakulima watakuwa wanahangaika tu bila mafanikio” amesema Dkt. Haule.
Dkt. Haule amesema kwa kuzingatia kanuni na miongozo itawasaidia wakulima kuepusha hasara, kupunguza magonjwa ya mimea na kuongeza mavuno kwa ekari, jambo ambalo litawawezesha wakulima kunufaika zaidi na jasho lao.
Dkt. Haule amesema Serikali imetenga fedha nyingi kwa ajili ya ruzuku katika zao la tumbaku hivyo amewasisitiza wadau wote kusimamia miongozo ya kitaalamu ya kilimo cha tumbaku kuanzia kupanda, utunzaji, uvunaji, ukusanyaji wa tumbaku ili kupata tumbaku bora inayokidhi viwango vya ndani na nje ya nchi.
Lengo la mkutano huo wa wadau ni kuboresha uzalishaji wa tumbaku, kuboresha upatikanaji wa masoko na ustawi wa wakulima wa zao hilo na kutafuta suluhu ya changamato zinazoikabili kilimo cha tumbaku katika Mkoa wa Mara.
Mhe. Haule ametumia fursa hiyo kukemea tabia ya utoroshaji wa tumbaku kuelekea nchi jirani na kuwatahadhalisha wadau hao kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa watakaobainika kutorosha tubaku katika Mkoa wa Mara.
Aidha, Dkt. Haule amewataka wanunuzi wa tumbaku na taasisi zinazotoa pembejeo kutoa elimu sahihi na endelevu kwa wakulima wa zao la tumbaku ili wakulima waweze kufaidika na kilimo cha tumbaku na kuendeleza uchumi wao binafsi na Taifa lao.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wakulima wa Mara Cooperative Union (WAMACU) LTD Bwana Momanyi Range ameomba ushirikiano baina ya Serikali, wakulima na wataalam ili zao la tumbaku liweze kuwa na tija kwa pande zote.
Bwana Range amesema kwa sasa wakulima wameitikia kulima tumbaku na hususan katika Wilaya ya Serengeti na kuwaomba wadau kuendelea kutoa elimu ili wakulima waweze kuboresha uzalishaji wa tumbaku na wananchi wengi zaidi waweze kulima tumbaku katika Mkoa wa Mara.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Postal Address: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Telephone: +255282622305
Mobile:
Email: ras.mara@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Mara Region . All rights reserved.