Idara ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu leo tarehe 26 Mei, 2025 imeanza kutoa mafunzo ya siku tatu kwa Kamati za wataalamu na Kamati Elekezi za Maafa kwa lengo la kufanya maandalizi ya kukabiliana na maafa katika Mkoa wa Mara.
Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Ndugu Gerald Musabila Kusaya amesema mafunzo hayo yamekuja katika wakati muafaka baada ya kutokea maafa katika Manispaa ya Musoma yaliyosababishwa na mvua na upepo tarehe 23 Machi, 2025.
“Wakati wa maafa ya Musoma, kulikuwa na sintofahamu nyingi kuhusu namna bora ya kukabiliana na maafa hayo na mafunzo haya yanakuja kutuandaa tuwe tayari kuyakabili pindi maafa yakitokea tena” amesema Bwana Kusaya.
Bwana Kusaya amewataka washiriki wa mafunzo hayo kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo kwa kuchangia maoni, kuuliza maswali na kuwa wasikivu wakati wa mafunzo hayo ili kupata uelewa wa namna ya kukabiliana na maafa.
Katibu Tawala wa Mkoa amesema baada ya mafunzo hayo, washiriki watatakiwa kwenda kutoa elimu katika Halmashauri, kwa wasaidizi sehemu za kazi na maeneo yao ya utawala ili kupanua zaidi elimu hiyo kwa wataalamu na viongozi walio chini yao.
Bwana Kusaya amewataka washiriki kutoa muda wao kwa hizi siku tatu ili kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo yatakayowasaidia kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi pindi majanga yatakapotokea.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Maafa katika Ofisi ya Waziri Mkuu Kanali Selestine Masalamado ametoa pole kwa maafa yaliyotokea Manispaa ya Musoma tarehe 23 Machi, 2025 na pongezi kwa hatua za haraka zilizochukuliwa kukabiliana na maafa hayo.
Kanali Masalamado amesema moja ya majukumu ya Idara ya Maafa ni kutoa elimu kwa kamati za maafa katika ngazi za Mikoa na Wilaya ili kukabiliana na maafa yaliyopo na yanayotegemewa kuwepo.
Kanali Masalamado amesema mafunzo haya yataongeza uwezo wa kamati hizi kukabiliana na maafa kitaalamu na kwa kufuata sheria, taratibu na miongozo ya kukabiliana na maafa pale yatakapotokea.
Kwa upande wake, Mratibu wa Maafa kutoka Idara ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu Bibi Doroth Pantaleo amesema amesema mafunzo hayo ni muhimu kwani yanajenga uelewa wa nini cha kufanya kabla na baada ya maafa kutokea.
Bibi Pantaleo amezitaja sababu za kuweza kuathiriwa na majanga na hivyo kusababisha maafa katika jamii kuwa ni pamoja na kutokujua, uharibifu wa mazingira, kuwa karibu na eneo la janga, umaskini, matatizo ya kijamii, mabadiliko ya tabia nchi.
Bibi Pantaleo amesema kuna majanga ya yanayotokana na nguvu za asili na majanga yanayosababishwa na shughuli za binadamu na kwa Tanzania majanga mawili yanasumbua mara kwa mara ambayo ni ukame na mafuriko.
Amesema baadhi ya majanga yanaweza kudhibitiwa na kutoa mfano wa bwawa la Kitaji ambalo mara nyingi limekuwa likisababisha mafuriko katika Manispaa ya Musoma na kusema kuwa linaweza kudhibitiwa kitaalamu baada ya kufanyiwa upembuzi yakinifu.
Bibi Pantaleo amesema matokeo ya kutokea kwa maafa katika jamii ni vifo, uhalibifu wa mali, kuteteleka kwa uchumi, ulemavu wa kudumu, hupanua uwigo wa umaskini na kusababisha baadhi ya waathirika kuwa wategemezi.
Washiriki wa mafunzo hayo ni pamoja na Wakuu wa Wilaya, Kamati ya Usalama ya Mkoa na Menejimenti ya Sekretarieti ya Mkoa wa Mara, Taasisi za Umma zinazohusika na maafa na uokoaji na wadau wa maafa.
Katibu Tawala Mkoa wa Mara
Anwani ya Posta: 13 Barabara ya Boma, P.o.Box 299 Musoma, 31101 Musoma, Mara
Simu: +255282622305
Simu:
Barua pepe: ras.mara@tamisemi.go.tz
Hatimiliki©2017 Mkoa wa Mara.Haki Zote Zimehifadhiwa